Breaking News

Trump afungua hoteli karibu na White House


Mgombea urais wa chama cha Republican nchini Marekani Donald Trump ataachana na kampeni kwa muda na kufungua jumba lake la hoteli ya Trump International lililo hatua chache kutoka ikulu ya White House.
Bw Trump atakata utepe katika hafla hiyo ya kuzindua jumba hilo Washington DC kisha arejelee kampeni katika jimbo la Carolina Kaskazini.
Mpinzani wake Hillary Clinton atatumia siku yake hii, ya kuadhimisha miaka 69 tangu kuzaliwa kwake, akifanya kampeni jimbo muhimu la Florida.
Bw Trump ana habari njema kiasi kwamba kura ya maoni ya Bloomberg Politics inasema anaongoza kwa asilimia mbili katika jimbo hilo.
Zikiwa zimesalia chini ya wiki mbili hadi siku ya uchaguzi, anaendelea kuwa nyuma ya Bi Clinton kwenye kura za maoni katika majimbo mengine muhimu yanayoshindaniwa.
Hoteli hiyo ya Bw Trump imegharimu $212m (£173m) naimejengwa eneo lililokuwa na posta ya zamani mjini Washington.
Hiyo ndiyo hafla ya pili ya mauzo na utangazaji kwa mgombea huyo wiki hii.
Alitokea kwenye ukumbi wa mchezo wa gofu wa Doral karibu na mji wa Miami, Florida, siku ya Jumanne kujumuika na baadhi ya wafanyakazi wake wa asili ya Kilatino (Hispanic) ambao walisimulia kuhusu maisha yao wakifanya kazi naye.




No comments