Breaking News

Mwili wa Sitta kuwasili leo




MWILI wa Spika mstaafu wa Bunge, Samuel Sitta unatarajiwa kuwasili leo saa tisa alasiri kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) jijini Dar es Salaam.

Taarifa iliyotolewa jana na Idara ya Habari (MAELEZO) ilieleza kuwa mwili huo unatarajiwa kupokewa na viongozi mbalimbali wa kitaifa wa Serikali na Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Kwa mujibu wa ratiba hiyo, baada ya kupokewa kwenye uwanja wa ndege, mwili huo utapelekwa nyumbani kwake Masaki jijini Dar es Salaam.

Aidha, taratibu za viongozi mbalimbali na wanaombolezaji kutoa heshima za mwisho kwa mwili wa marehemu zitafanyika kwenye Viwanja vya Karimjee kesho kuanzia saa 1:30 asubuhi.

Baada ya kukamilika kwa ratiba hiyo, mwili wa Sitta utapelekwa JNIA kwa ajili ya kusafirishwa kwenda Dodoma.

Taarifa ilisema mwili huo utawasili Dodoma saa nane mchana na kupokewa na viongozi mbalimbali wa Mkoa wa Dodoma na Bunge.

Baadaye mwili huo utapelekwa katika Viwanja vya Bunge ambako salamu mbalimbali zitatolewa na Spika, Waziri Mkuu, Kambi Rasmi ya Upinzani na viongozi wa Mkoa wa Dodoma.

No comments