Breaking News

Bulaya,Wassira ngoma bado itaendelea.

Baada ya Mahakama Kuu, Kanda ya Mwanza kutupilia mbali maombi ya wananchi wanne wa kutaka itengue ushindi wa Mbunge wa Jimbo la Bunda Mjini Ester Bulaya (Chadema), walalamikaji hao wamesema watakata rufaa katika Mahakama ya Rufaa kwa kile walichosema kuwa Mahakama hiyo haikutenda haki katika kutoa maamuzi hayo.

Novemba 18, mwaka huu, Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza iliyokuwa inasikiliza kesi hiyo namba moja ya mwaka huu, katika Mahakama ya Mkoa wa Mara mjini Musoma, chini ya Jaji Noel Chocha, ilitupilia mbali kesi hiyo na kumthibitisha Bulaya kuwa ni Mbunge halali wa jimbo hilo.

Wananchi hao wanne walikuwa wamefungua kesi hiyo wakipinga ushindi wa Bulaya dhidi ya Stephen Wasira kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), katika uchaguzi mkuu uliofanyika mwaka jana.

Baada ya hukumu hiyo kutolewa waandishi wa habari walimhoji mmoja wa walalamikaji Janes Ezekiel, ambaye alisema kuwa watakaa na wenzake waone namna ya kukata rufaa.

Hata hivyo baadaye mlalamikaji mwingine Ascetic Malagila alimwambia mwandishi wa habari hii kuwa tayari wamekubaliana na wenzake pamoja na mwanasheria wao kuwa watakata rufaa katika Mahakama ya Rufaa kupinga hukumu hiyo, kwa kile alichoeleza kuwa wameshindwa kwa sababu ya uonevu na kwamba watatafuta haki yao katika Mahakama ya Rufaa.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, Wasira alidai kuwa tayari walalamikaji hao pamoja na wakili wao Constantine Mutalemwa, wamekutana na kukubaliana kukata rufaa katika Mahakama ya Rufaa kutafuta haki.

Kabla ya hukumu hiyo kutolewa Jaji Chocha, alirejea baadhi ya vifungu vya sheria pamoja na hoja mbalimbali zilizotolewa na waleta maombi (walalamikaji) na wajibu maombi wa kwanza, wa pili na watatu.

Jaji Chocha alisema kuwa kutokana na kupitia vifungu vyote vya sheria pamoja na ushahidi uliotolewa na waleta maombi katika Mahakama hiyo, ni kwamba ushahidi wao haujajitosheleza katika hatua ya kutengua ubunge wa jimbo hilo.

No comments